Ijue Taasisi ya Nyaraka na Kumbukumbu Zanzibar..
Taasisi ya Nyaraka na Kumbukumbu imeanzishwa na inatekeleza majukumu yake kupitia Sheria ya Kuanzishwa kwa Taasisi ya Nyaraka na Kumbukumbu Zanzibar Nam. 3, 2008. Jukumu kuu la Taasisi ni kutunza na kuhifadhi kumbukumbu na nyaraka za Serikali kama Urithi wa Taifa. Pia kusimamia kumbukumbu zote zinazozalishwa na kuhifadhiwa katika taasisi na mashirika ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, pamoja na taasisi na mashirika ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa ofisi zake zilizopo Zanzibar.
Shughuli za uhifadhi na utunzaji wa Nyaraka na Kumbukumbu Zanzibar ulianza mwanzoni kabisa mwa karne ya 20. Na mnamo mwaka 1925 Ilitengwa sehemu maalumu ya kuhifadhia nyaraka na kumbukumbu za Serikali katika Jumba la Makumbusho ya Amani (Beit al Aman Peace Memorial Museum) liliopo eneo la Mnazi Mmoja, Unguja. Dkt. Spurrier alikuwa ni Mkuu wa Makumbusho (Principal Curator) wa mwanzo kwa Makumbusho ya Amani (Beit al Aman Peace Memorial Museum -1925 – 1955) na alisimamia shughuli za uhifadhi na utunzaji wa nyaraka pamoja na Makumbusho na Mambo ya Kale.
Katika mwaka 1954 ilipitishwa Kanuni ya Serikali iliyosisitiza umuhimu wa uhifadhi na utunzaji wa nyaraka na makumbusho. Mwaka 1955 Serikali ya Kikoloni ilimuajiri mtaalamu wa kuhifadhi nyaraka Bw. Thompson, kama ni Muhifadhi Mkuu wa Nyaraka za Serikali (Chief Government Achivist) wa mwanzo Zanzibar (1955 – 1963) kazi yake ilikuwa ni kusimamia shughuli za uhifadhi na utunzaji wa nyaraka za Serikali ya Zanzibar.
Ujenzi wa jengo maalumu la kuhifadhia nyaraka ulianza rasmi mwaka 1957 na kukamilika mwaka 1963. Baadae nyaraka zote zilizokuwa zimehifadhiwa kwenye Jumba la Makumbusho ya Amani zilihamishiwa katika Jengo la Nyaraka la Kilimani ambalo hadi sasa linatumika kwa madhumuni hayo. Ingawaje, kazi za makumbusho na mambo ya kale ziliendelea kusimamiwa kwa pamoja na za nyaraka. Mwanzoni mwa mwaka 2007 Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar iliamua kuzitenganisha shughuli za uhifadhi na utunzaji wa nyaraka na zile za Makumbusho na Mambo ya Kale kuwa idara mbili (2) tofauti kimamlaka na kimajukumu.
Aidha, Sheria ya Kuanzishwa kwa Taasisi ya Nyaraka na Kumbukumbu Zanzibar Namba 3 ya mwaka 2008 ilipitishwa na kufuta matumizi ya Sheria iliyoanzisha Idara ya Nyaraka, Makumbusho na Mambo ya Kale.
Dira
Kuwa na mfumo bora wa Usimamizi, Utunzaji na Uhifadhi wa Nyaraka na Kumbukumbu ili kutoa huduma bora kwa Umma na kuendeleza Urithi wa Kihistoria wa Zanzibar.
Dhamira
Kuimarisha taratibu, miongozo na mipango maalum itakayohakikisha viwango bora vya usimamizi, utunzaji na uhifadhi wa Nyaraka na Kumbukumbu.
Lengo kuu la Taasisi ni kusimamia, kutunza na kuhifadhi Nyaraka na Kumbukumbu kwa matumizi ya Serikali na umma.
- Kusimamia utunzaji na uhifadhi bora wa mifumo ya usimamizi wa kumbukumbu na nyaraka katika taasisi za umma
- Kutoa miongozo na ushauri wa kumbukumbu na nyaraka zitakazokuwa hazina thamani ya kudumu na zinahitaji kuteketezwa au kuharibiwa
- Kukagua na kusimamia miongozo na taratibu za uhamishaji wa kumbukumbu na nyaraka zenye thamani ya kuhamishiwa katika Jumba la Nyaraka au Kituo cha Uhifadhi wa Kumbukumbu kama Sheria hii inavyoelekeza
- Kufanya matengenezo ya nyaraka (Restoration of Archival Documents) muhimu na za kipekee zilizochakaa au kupoteza uhalisia wake kithamani
- Kutoa huduma za utafiti na ushauri elekekezi kwa watafiti na jamii kwa nyaraka zilohifadhiwa katika Jumba la Nyaraka au Kituo cha Uhifadhi Kumbukumbu kwa chini ya mamlaka ya Mkurugenzi.